Mtoto Wa Afrika! Poem by Fadhy Mtanga

Mtoto Wa Afrika!

Rating: 5.0

Upo huko mashambani,
Kwenye mazingira duni,
Nani anakuthamini,
Akupeleke shuleni?
Mtoto wa Afrika!

Wahenyeka migodini,
Umezama taabuni,
Hunayo matumaini,
Hujui ‘takula nini,
Mtoto wa Afrika!

Unateseka vitani,
Na bunduki mabegani,
Wanakufundisha nini,
Maisha yako usoni?
Mtoto wa Afrika!

Watendwa mwako mwilini,
Na jitu zima fulani,
La miaka hamsini,
Ukimbilie kwa nani?
Mtoto wa Afrika!

Waondolewa shuleni,
Ukaolewe mjini,
Nani anakuthamini,
Akubakize shuleni?
Mtoto wa Afrika!

Mahali barabarani,
Una kopo mkononi,
U ombaomba jamani,
Sisi wala hatukwoni,
Mtoto wa Afrika!

Wasikia radioni,
Wenzako matamashani,
Na viongozi fulani,
Umebaki mtaani,
Mtoto wa Afrika!

Uliko ni kijijini,
Shuleni waketi chini,
Wenzako huku mjini,
Leo wapo jukwaani,
Mtoto wa Afrika!

Utangoja hadi lini?
Tateseka hadi lini?
Utakombolewa lini?
Utafurahia lini?
Mtoto wa Afrika!

Majibu anayo nani?
Mtoto yupo shidani,
Anakula jalalani,
Twapaswa kumthamini,
Mtoto wa Afrika!

Kwani tunafanya nini?
Na kwa faida ya nani?
Tunajenga kitu gani,
Pasipo kumthamini?
Mtoto wa Afrika!

Tupo usingizini,
Tuamke sasa!

COMMENTS OF THE POEM
READ THIS POEM IN OTHER LANGUAGES
Fadhy Mtanga

Fadhy Mtanga

Dar es Salaam, Tanzania
Close
Error Success